Hujjatul Islam Hamid Shahriari alisema hayo warsha iliyofanyika kwa njia ya intaneti chini ya anuani ya “Operesheni ya Kimbunga cha Al-Aqsa; Mwanzo wa Mwisho wa Utawala wa Kizayuni”, ambayo iliandaliwa Jumatano na WFPIST.
Amesema ulimwengu wa Kiislamu unapitia nyakati ngumu siku hizi kwa kuzingatia yale wanayokabili watu madhulumu wa Palestina katika Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Ameongeza kuwa, hivi leo thamani za Uislamu na za kambi ya mabeberu duniani zinakabiliana katika sehemu mbalimbali za dunia ikiwemo huko Gaza.
Wananchi Wapalestina wanaodhulumiwa wa Gaza wanakabiliana na utawala wa mauaji ya watoto ambao hauna huruma kwa raia na unajaribu kuendelea kupora ardhi ambayo si yake kupitia mauaji na uhalifu usiokoma.
Kinyume na dhulma hii kubwa inayofanywa na kiburi cha ulimwengu, Uislamu umesisitiza thamani ya uadilifu, ukitufundisha kufuata haki hata kama ni kinyume chetu, alisema.
Hujjatul Islam Hamid Shahriari ameongeza kuwa, ni wajibu kwa Waislamu kuwasaidia wanaodhulumiwa na kuwaokoa na dhulma.
"Leo tuko katika kipindi cha mabadiliko ya kihistoria ambapo wanyonge watatawala ulimwengu na kupata tena haki zao," alisema.
Mwanazuoni huyo mwandamizi wa Iran aliongeza kuwa leo ni wakati wa vitendo sio maneno.
"Ni wajibu kwa watawala wa nchi za Kiislamu kuungana na kukimbilia kuisaidia Palestina katika uwanja wa utekelezaji," alisisitiza.
Matamshi yake yametolewa huku utawala wa Israel ukiendelea na mashambulizi yake ya anga dhidi ya Gaza yaliyoanza karibu wiki tatu zilizopita.
Mashambulizi hayo yamepelekea Wapalestina 6,000, wakiwemo wanawake na watoto kupoteza maisha, huku zaidi ya watu 18,000 wakijeruhiwa.
Mashambulizi hayo ya anga yanafuatia operesheni ya ghafla iliyopewa jina la Operesheni ya Kimbunga cha Al-Aqsa iliyoanzishwa na Hamas dhidi ya utawala katili wa Israel mnamo Oktoba 7.
Hamas imesema operesheni hiyo ilitekelezwa kwa ajili ya kukabiliana na ukatili wa utawala huo ghasibu katika maeneo yanayokaliwa kwa mabavu na ukiukaji wake wa matukufu ya Msikiti wa Al-Aqsa.
348574