Katika mkutano huo ambao umefanyika Jumanne katika ubalozi wa Iran mjini Doha, Amir-Abdollahian amesisitiza kuwa Iran itaendelea kuunga mkono haki za watu wa Palestina wanaopamabana na utawala ghasibu wa Israel.
Amir- Abdollahian amesema kwa mujibu wa sera za kimsingi za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, kadhia ya Palestina ni tatizo ambalo limeibuliwa katika kitovu cha umma wa Kiislamu. Amesema matatizo ya Palestina yanatokana na utawala wa Kizayuni unaoua watoto na ambao unapata himaya ya nchi za Magharibi.
Amir-Abdollahian ameendelea na mazungumzo yake kwa kulaani jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya Mji wa Quds (Jerusalem), Msikiti wa Al Aqsa, Ukanda wa Ghaza na maeneo mengine ya ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu. Hali kadhalika amelaani jinai za Wazayuni dhidi ya taifa la Palestina na matukufu yake.
Katika mazungumzo hayo, Ismail Haniya, Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Hamas ameishukuru tena kwa dhati Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kutokana na uungaji mkono wake kwa mapambano ya taifa la Palestina dhidi ya utawala wa Kizayuni. Aidha ametoa wito kwa nchi zote za Kiislamu, Kiarabu na jamii ya kimataifa kwa ujumla kuchukua hatua za kivitendo za kukabiliana na jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel.