Ayatullah Muhammad Emami-Kashani ameyasema hayo katika hotuba za Swala ya Ijumaa ambapo sambamba na kueleza kwamba, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran yaliyofikia kileleni tarehe 22 Bahman 1357 Hijiria Shamsia, sawa na tarehe 11 Februari 1979, yamezuia malengo machafu na haribifu ya mabeberu, amebainisha kuwa, ushindi wa mapinduzi hayo nchini uliwahamasisha wakazi wa kanda hii na nchi za Kiislamu kusimama imara kwa ajili ya kukabiliana na njama za Wazayuni na Wamarekani.
Khatibu wa Swala ya Ijumaa iliyoswaliwa leo mjini Tehran amesisitiza kwamba, mpango wa Muamala wa Karne ni fedheha na kudhalilika kwa karne Marekani na utawala khabithi wa Israel. Amesema wakazi wa kanda hii ya magharibi mwa Asia pamoja na Wapalestina watasimama imara kukabiliana na mpango huo wa Kimarekani na Kizayuni.
Hivi karibuni Rais Donald Trump wa Marekani alizindua mpango huo ambao unajumuisha vipengee kadhaa ikiwa ni pamoja na kutwaliwa mji wote wa Quds na vitongoji vya walowezi katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan sambamba na kufumbia macho haki ya kurejea Wapalestina katika ardhi zao za asili.