Familia yake imewaambia waandishi habari kuwa, maafisa wa kijasusi wa utawala wa Israel waliihujumu nyumba ya Sheikh Sabri na kumfahamisha kuwa amekamatwa.
Imedokezwa kuwa mwanazuoni huyo wa ngazi za juu wa Palestina amepelekwa katika kituo cha polisi cha al-Qashla Quds Magharibi
Mwezi Januari, wakuu wa utawala haramu wa Israel walimpiga marufuku Sheikh Ekrima Sabri kuingia katika Msikiti wa Al Aqsa mjini Quds kwa muda wa miezi minne.
Sheikh Sabri mara kwa mara amekuwa akiashiria uporaji wa ardhi za Wapalestina katika mji mtakatifu wa Quds unaokaliwa kwa mabavu kwa ajili ya kujenga na kupanua vitongoji vya walowezi wa Kizayuni na kuonya kuhusiana na matokeo mabaya na hatari ya njama za kuupa sura ya Kiyahudi mji huo mtakatifu.
Sheikh Sabri pia hulaani vitendo vya utawala haramu wa Israel vya kubomoa kila leo nyumba za wananchi madhulumu wa Palestina na kuitaja hatua hiyo kuwa ni ya kibaguzi na kidhulma ambayo inapaswa kupingwa kwa nguvu zote.
Khatibu wa Masjidul Aqswa amekuwa mstari wa mbele kuyataka mataifa yote ya Kiislamu na Kiarabu kuingia uwanjani kwa ajili ya kukabiliana na uamuzi wa Marekani wa kutaka kuuhamishia ubalozi wake katika mji wa Quds.