IQNA

Darul Iftaa ya Misri: Saumu huimarisha kinga mwilini na haisababishi kuambukizwa corona

19:05 - April 15, 2020
Habari ID: 3472668
TEHRAN (IQNA) – Darul Iftaa ya Misri imetoa taarifa na kusisistiza kuwa: “Baada ya kushauriana na kamati ya madaktari tumefikia natija kuwa, saumu haichangii katika kuambukizwa corona (COVID-19).”

Kwa mujibu wa taarifa katika tovuti ya youm7, Darul- Iftaa ya Misri imesambaza taarifa katika ukurasa wake rasmi wa Facebook na kuandika kuwa: “Tumeshauriana na kamati ya madaktari na kufikia natija kuwa, saumu haihusiki katika kuambukizwa corona na kwamba saumu husaidia kuimarisha zaidi kinga ya mwili katika kukabiliana na corona.”

Taarifa hiyo imeongeza kuwa: “Iwapo saumu itakuwa na madhara kwa wagonjwa, madaktari na wauguzi ambao wako katika hatari ya kuambukizwa corona basi saumu kwao haijuzu.”

Aidha taarifa hiyo imesema saumu kwa walioambukizwa corona itategemea ushauri wa madaktari. “Iwapo daktari atashauri kuwa saumu kwa aliyeambukizwa itakuwa na madhara basi kutekeleza ushauri wa daktari ni wajibu kwa sababu kulinda afya kunapewa kipaumbele zaidi ya saumu,” imesema taarifa hiyo ya Darul Iftaa ya Msiri.

Mwezi Mtukufu wa Ramadhani umetabiriwa kuanza tarehe 25 Aprili na Waislamu maeneo mbali mbali ya dunia  wanajitayarishwa kwa saumu huku janga la corona likiwe limeenea duniani.

3891913

captcha