Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanyika, kumekithiri matamshi na vitendo vya chuki dhidi ya Waislamu kabla ya uchaguzi mdogo wa bunge uliopangwa kufanyika Novemba sita. Wanahusika wanaeneza hofu kuhusu wahajiri Waislamu nchini humo. Kwa mujibu wa Scott Simpson, mkurugenzi katika shirika la kuwatetea Waislamu la Muslim Advocates ambalo limeandika ripoti hoiyo, kuna wanasiasa wanaowapinga Waislamu katika maeneo yote ya Marekani. Ripoti hiyo imeorodhesha kesi 80 kote za Marekani za wagombea ambao wamekuwa wakieneza chuki dhidi ya Waislamu katika kipindi cha miaka miwili iliyopita. Ripoti hiyo imebaini kuwa, aghalabu ya wanaoeneza chuki dhidi ya Waislamu na Uislamu ni wagombea wa chama cha Republican cha Rais Trump.
Kwa ujumla kote Marekani kulishuhudiwa ongezeko la chuki dhidi ya Waislamu na hilo linatokana na sera za kibaguzi za Trump.
Wakati wa kampeni zake, Trump alikuwa ametaka Waislamu wazuiwe kikamilifu kuingia Marekani.
Baraza La Mahusiano ya Kiislamu Marekani (CAIR) linasema tokea Donald Trump achaguliwe kuwa rais wa Marekani, Waislamu nchini humo wameshuhudia ongezeko kubwa la ubaguzi dhidi yao huku wakishambuliwa na kubugudhiwa na watu wenye chuki dhidi ya Uislamu.