Katika taarifa iliyotolewa Jumapili, Wizara ya Wakfu na Masuala ya Kidini ya Oman imesema kwa mujibu wa makadirio ya mwezi mwandamo, itakuwa haiwezekani kuona hilali ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani mnamo Jumanne Mei 15, 2018 inayosadifiana na 29 Shaaban mwaka 1439 Hijria Qamaria,( kwa mujibu wa mahesabu ya Oman). Kwa msingi huo Mei 16, Mwezi wa Shaaban utatimiza siku 30 na Mei 17 itakuwa siku ya kwanza ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani mwaka 1439 Hijria Qamaria.
Kwa kawaida Oman huwa inajitegemea katika kutangaza kuanza au kaumalizika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na haifuati nchi zingine za Ghuba ya Uajemi ambazo aghalabu huiga Saudi Arabia.
Wizara ya Wakfu na Masuala ya Kidini Oman imewatakia Waislamu wote duniani kheri na fanaka katika Ibada ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Katika kuanza au kumalizika Mwezi Mtukufu wa Ramadahni, baadhi ya Waislamu au nchi za Kiislamu hutegemea kuuona mwezi na baadi hutegemea mahesabu ya kinujumu.