IQNA

Waislamu Kenya wapinga kuteuliwa balozi asiyekuwa Mwislamu kuwakilisha nchi hiyo Saudia

14:35 - August 05, 2018
Habari ID: 3471620
TEHRAN (IQNA)- Waislamu nchini Kenya wamepinga hatua ya Rais Uhuru Kenyatta wa nchi hiyo kumteua mwanadiplomasia asiyekuwa Mwislamu kuwa balozi wa nchi hiyo Saudi Arabia.

Khatibu wa mskiti wa Jamia jijini Nairobi Sheikh Muhammed Swalihu na mwenyekiti wa Baraza Kuu la Waislamu Kenya, SUPKEM, Balozi Yusuf Nzibo wametoa wito kwa Rais Kenyatta kubatilisha uteuzi wa aliyempendekeza kuwa balozi wa Kenya nchini Saudia, Peter Ogego, na badala yake achague Mwislamu kuchukua nafasi hiyo kwa mujibu wa utaratibu ambao umekuwepo.

Viongozi hao wa Waislamu wamesema kuteua balozi Mwislamu Saudi Arabia itakuwa bora zaidi kwa sababu ya kutoa huduma kwa Wakenya wanaofika nchini humo kutekeleza ibada ya Hija au Umrah. Wamesema hilo ni muhimu kwa kuzingatia kuwa wasiokuwa Waislamu hawaruhusiwi kuingia katika mji matakatifu ya Makka.

Iwapo Bunge la Kenya litamuidhinisha Ogego, basi atachukua mahala pake gavana wa Wajir Mohammed Abdi Mohamud ambaye alikuwa kama balozi wa Saudi Arabia 2014.

Balozi Nzibo ambaye aliwahi kuwa balozi wa Kenya katika nchi za Marekani , Uholanzi na Saudi Arabia katika nyakati tafauti, amemwandikia barua Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na kumkabidhi rasmi malalamiko ya Waislamu kuhusiana na suala hilo. Hadi sasa serikali ya Kenya haijatoa taarifa kuhusiana na uteuzi huo ulioibua utata.

3735799

captcha