Taarifa zinasema Waislamu 309 walioikumbatia dini tukufu ya Kiislamu katika miaka ya hivi karibuni kutoka nchi 20 walishiriki katika mashindano hayo ambayo yanafanyika kwa mwaka wa pili.
Mashindano hayo yaliandaliwa na Taasisi ya Kiislamu ya Al-Malumat inayofungamana na Jumuiya ya Dar-al-Birr ya UAE.
Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Rashid Junaibu amesema mashindano hayo yanalenga kuimarisha mafungamano ya waliosilimu na Qur'ani Tukufu na kuwahimiza kuhifadhi Qur'ani sambamba na kutafakari kuhusu misingi na mafundisho yake.
Aliongeza kuwa, karibu asilimia 50 ya washiriki wa mwaka huu pia walishiriki katika duru kwanza ya mashindano hayo.
Wafanyakazi kutoka mabara ya Asia, Ulaya, Afrika na Amerika wanaoishi UAE walishiriki katika mashindano hayo.
Mashindano hayo yamefanyika katika kategoria za kuhifadhi na kusoma Qur'ani Tukufu. Washindi walitunukiwa zawadi baada ya kumalizika mashindano ambapo miongoni mwa zawadi walizopata ni tikiti ya kutekeleza Ibada ya Umrah.