IQNA

Kongamano la Umoja wa Kiislamu Tehran lamalizika kwa kuunga mkono Intifadha ya Palestina

19:49 - December 08, 2017
Habari ID: 3471300
TEHRAN (IQNA)- Mkutano wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu umemalizika mjini Tehran kwa kutoa taarifa yenye vipengee 26 inayosisitiza kuimarishwa umoja wa Kiislamu kwa ajili ya kupambana na njama za maadui, ikiwemo njama mpya ya Marekani dhidi ya Quds Tukufu.

 

Mkutano huo ulioanza siku ya Jumanne mjini Tehran ulimalizika Alkhamisi usiku ambapo kuwalikuwa na wanazuoni, wanafikra na wanasiasa wa madhehebu ya Shia na Sunni walioshiriki kutoka kila kona ya dunia. Tarifa ya mwisho ya mkutano huo imezingatia masuala mawili muhimu. La kwanza ni kuwa, kwa kutilia maanani uwezo mkubwa wa Ulimwengu wa Kiislamu, kuhuishwa ustaarabu wa Kiislamu kwa lengo la kuokoa jamii ya mwanadamu kutokana na machungu anayoyapitia ni jambo la dharura. Suala la pili ni kulaaniwa hatua iliyochukuliwa hivi karibuni na Rais Donald Trump wa Marekani ya kuutambua mji mtakatifu wa Quds kuwa mji mkuu wa utawala haramu wa Israel. Washiriki wa Mkutano wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu mjini Tehran wamesisitiza udharura wa kukabiliana na siasa mpya za Marekani za kuuyahudisha mji mtakatifu wa Quds na kudhibiti matukufu ya Waislamu na kusisitiza kuwa Ulimwengu wa Kiislamu inahitajia Intifadha ya Palestina kwa ajili ya kukabiliana na njama mpya ya maadui dhidi ya Beitul Maqdis.

Taarifa hiyo pia imebainisha kusikitishwa na mauaji na uharibifu unaojiri katika baadhi ya nchi za Kiislamu kama Afghanistan, Iraq, Syria na Yemen na kuzitaja baadhi ya serikali na mirengo katika Ulimwengu wa Kiislamu ambayo inatekeleza njama za kufanikisha malengo ya kibeberu na ya Uzayuni kuwa chanzo cha masaibu na mashaka hayo yote yanayowakumba Waislamu katika nchi hizo. 

Duru ya 31 ya Kongamano la Kimataifa la Wiki ya Umoja wa Kiislamu ilifanya hapa Tehran kuanzia tarehe 5 hadi 7 mwezi huu wa Disemba ambayo ni sawa na tarehe 16 hadi 18 Rabiul Awwal 1439 Hijria. 

 

3467009

captcha